Thursday, December 29, 2011

MSICHANA WA MIAKA 9 AFARIKI BAADA YA KUTAHIRIWA


Ngariba wa miaka 70, mkazi wa kijiji cha Irienyi Kinesi, wilayani Rorya, mkoa wa Mara, Nyaisanga Marwa, amekamatwa na Polisi na anatarajia kufikishwa mahakamni kujibu mashitaka ya kumkeketa mwanafunzi wa darasa la pili wa Shule ya Msingi Irienyi (jina tunalihifadhi) na kumsababishia kifo, baada ya kutokwa na damu nyingi kwenye sehemu aliyokatwa.

Kamanda wa Polisi wa Kanda ya Tarime/Rorya, Justus Kamugisha, jana alisema kuwa, tukio hilo lilitokea Desemba 19, mwaka huu, katika kijiji cha Irienyi Kinesi, wilaya ya Rorya na kwamba baada ya mtoto huyo kukeketwa, alitokwa damu nyingi iliyoendelea kutoka bila msaada wowote kwa matumaini kuwa atapona kwa miti shamba.

Kamanda huyo alisema, Desemba 23, mwaka huu, mtoto huyo (9) alipoteza maisha na kwamba Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na ndugu wa marehemu walimkamata ngariba huyo kabla hajatoroka na hadi sasa yupo mikononi mwa Polisi na wanatarajia kumfikisha mahakamani wakati wowote kujibu shitaka la kukeketa na kusababisha kifo.